08/31/2026 | News release | Distributed by Public on 08/31/2026 06:44
Oksana, mwanamke kutoka Mariupol, ni muuguzi. Alizaliwa nchini Ukraine na ameishi Mariupol tangu kuzaliwa, ingawa familia yake asili inatoka eneo la Samara nchini Urusi. Kwa hivyo, ingawa Oksana alikuwa na pasipoti ya Ukraine, alijiona kuwa Mrusi.
Ndio maana katika mwaka wa 2014, wanajeshi wa Ukraine waliojeruhiwa wakipigana dhidi ya jaribio la Urusi la kuteka eneo la Donetsk walipoletwa katika chumba cha upasuaji katika hospitali aliyokuwa akifanya kazi, alianza kuwachukia.
Leo, Oksana anawachukia Warusi walioivamia Mariupol yake ya asili katika mwaka wa 2022 kwa kiwango kilekile. Badala ya kuleta furaha na ustawi aliokuwa akitarajia, waliharibu kila kitu alichokithamini.
'Maisha yangu yote leo yamejaa kukata tamaa. Sasa ninafanya kazi katika hospitali mbili, karibu saa 16 kwa siku, ili tu nisione kinachoendelea karibu nami. Najichosha kupita kiasi, narudi nyumbani, naingia katika jengo ambalo madirisha yake bado yamefunikwa kwa mbao, ambako hakuna umeme na usambazaji wa waji sio wa kutegemewa, kisha nalala hadi asubuhi. Hivi ndivyo nimeishi kila siku kwa miaka michache iliyopita. Ni kama siku ya 'Groundhog Day', na sioni njia ya kutoka," anasema.
Hadithi nyingi kama hizo zinaweza kusikika katika Mariupol inayovamiwa na Urusi. Watu hawazisimulii mitaani; ni hatari mno. Lakini huzijadili ndani ya nyumba zao zilizoharibiwa.
'Sasa tunaishi katika hali ambayo tunaogopa kusema chochote kwa sauti. Hata sizungumzi na majirani zangu kwa sababu sijui wanachofikiria kwa kweli. Nilikubali kuzungumza nawe kwa sababu tu tumefahamiana kwa miaka mingi,' Oksana anatuambia.
Haangalii televisheni wala kusoma magazeti yanayosambazwa bila malipo na mamlaka za uvamizi. Vyombo hivyo vinawasilisha taswira iliyopotoshwa ya uhalisia ambayo inatofautiana sana na ukweli kiasi kwamba, wakati mwingine, haisababishi hata hasira bali kicheko.
"Kujenga Upya"
Katika miezi ya kwanza ya uvamizi kamili, Detector Media - shirika la kiraia la Ukraine linalofuatilia ubora wa maudhui ya vyombo vya habari - ilibaini chaneli mpya 88 za ndani za Telegram zilizotumiwa na Urusi kuhalalisha uvamizi wake wa miji ya Ukraine. Mojawapo ya simulizi kuu za mtandao huo ilikuwa madai ya 'kujenga upya na kurejea katika maisha ya kawaida'. Mariupol ilipewa nafasi kubwa katika simulizi hilo.
Pamoja na chaneli za Telegram, chaneli za YouTube zilianza kujitokeza kwa wingi. Mamia ya wanablogu kutoka maeneo mbalimbali ya Urusi walisafiri hadi katika maeneo yaliyovamiwa ili kuionyesha dunia 'furaha ya kujenga upya'.
'Chaneli hizi zilitengenezwa kwa ajili ya Warusi, sio kwa ajili yetu,' Oksana anasema. 'Labda ilikuwa rahisi kwao kuamini. Lakini sisi tunaona uhalisia: Urusi ilibomoa majengo 640 ya ghorofa na kujenga 70 pekee, na kuwaacha watu wengi bila makazi. Kati ya nyumba 43,000 za watu binafsi, ilirekebisha 1,000 pekee. Hizi ni takwimu za mamlaka za uvamizi pekee.'
Oksana anamiliki nyumba katika wilaya ya Prymorskyi mjini Mariupol. Iliharibiwa vibaya wakati wa vita. Paa lilitoboka, na madirisha yakapasuliwa na mawimbi ya mlipuko. Oksana alijitahidi kadiri alivyoweza kufunika madirisha kwa mbao. Mwanawe mdogo alimsaidia kukarabati paa.
Mwanawe mkubwa, ambaye anasoma nje ya nchi, alirithi nyumba ya ghorofa huko Mariupol kutoka kwa nyanya yake. Oksana aliitunza wakati wote wa uvamizi, lakini mwezi mmoja uliopita alikuta ilani yenye muhuri ikitangaza kuwa nyumba hiyo haina mwenyewe na inapaswa kutwaliwa.
'Niliwasilisha kesi mahakamani, lakini kikao cha kusikiliza kesi hiyo kitafanywa baada ya miezi mitatu kwa sababu mahakama zimelemewa na kesi. Wakati huo huo, nyumba hiyo tayari imeorodheshwa kuwa "haina mwenyewe". Hii ni nyumba ya familia yetu, ambayo niliikarabati mwenyewe, lakini sasa wananiambia niondoke. Wanawezaje kuwatendea watu hivi na wakati huo huo kudai kuwa wamejenga upya Mariupol? Huu ni mwonekano wa nje tu; nyuma yake, kila kitu kimeteketezwa kabisa," Oksana anasema kwa uchungu.
"Maisha ya Kawaida"
Mwanamke mwingine tuliyezungumza naye, Maria, alibaki katika Mariupol iliyovamiwa kwa sababu ya mama yake mzee, ambaye ana umri wa miaka 87 na alikataa kabisa kuondoka jijini. Anasema anataka kufia mahali ambapo wazazi wake wamezikwa. Mume wa Maria pia alikataa kuondoka nyumbani kwao.
'Sitaki kukumbuka yale tuliyopitia katika majira ya mchipuko ya mwaka wa 2022. Mume wangu alikuwa amejeruhiwa. Sote tulipoteza kazi zetu kwa sababu tulifanya kazi katika Azovstal. Kiwanda hicho hakipo tena. Bado sijapata kazi. Mume wangu, ambaye ni mfanyakazi mwenye ujuzi wa chuma, sasa anafanya kazi za vibarua katika maeneo ya ujenzi. Anafanya kazi saa 12 hadi 14 kwa siku, akiwa na siku moja tu ya mapumziko kwa wiki - kama mtumwa - ili tu kuilisha familia yetu. Hivyo ndivyo 'ukombozi' unavyomaanisha kwetu. Wakati huo huo, Warusi wanaonekana katika kila chaneli ya televisheni wakimwambia kila mtu jinsi tulivyo na furaha kuishi nao hapa," Maria anasema.
Anadai kwamba katika miezi ya kwanza ya uvamizi, Urusi ilijaribu kununua uaminifu wa wakazi wa eneo hilo.
"Waliongeza pensheni, wakatoa malipo ya ziada na fidia. Sasa malipo hayo ya ziada yamesitishwa, na baadhi ya watu wameanza kupunguziwa pensheni zao. Lakini hawasemi hili kwenye televisheni.
Warusi waliahidi kuijenga upya Mariupol ndani ya miaka mitatu. Kisha tukaona kwenye televisheni kwamba Pushilin, mkuu wa utawala wa uvamizi ulioteuliwa na Kremlin, tayari alikuwa ameripoti kwa Putin kwamba jiji limejengwa upya. Kwa kweli, walikuwa wamepaka tu rangi sehemu za nje za majengo. Bado hakuna makazi. Nyumba za watu binafsi bado zimeharibiwa; hakuna mtu aliyewahi kuzirekebisha. Viwanda vimeharibiwa, na mbali na sekta ya huduma, hakuna kazi. Hali hii ndiyo wanayoita maisha ya kawaida."
'Kiwango cha ulevi hapa sasa ni cha kushtua. Nyakati za jioni, wanaume na wanawake hufunga milango ya nyumba zao - au za watu wengine - na kuanza kulewa kwa sababu hakuna jambo lingine la kufanya. Kila mtu aliyenusurika uvamizi anateseka kutokana na mshtuko wa kisaikolojia, lakini hakuna hata daktari mmoja wa magonjwa ya akili jijini. Kwa hivyo, kwa watu wengi, pombe imekuwa tiba pekee ya kila ugonjwa. Ni vigumu kuwahukumu,' anamalizia.
Inaonekana kuwa mashine ya propaganda haifanyi kazi pale ambapo uhalisia unatofautiana kwa kiasi kikubwa na kile kinachosemwa kwenye televisheni. Watu wanazidi kukata tamaa.